JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA

MAMLAKA YA MAWASILIANO TANZANIA

TAASISI YENYE VIWANGO VYA ISO 9001: 2015

TCRA na kampeni kabambe ya kuigeuza mitandao ya kijamii kuwa fursa


TCRA na kampeni kabambe ya kuigeuza mitandao ya kijamii kuwa...

 

Dunia inakwenda kasi, na teknolojia inazidi kuimarika watu wanahabarika kupitia mitandao ya kijamii.

Tanzania ni miongoni mwa nchi zilizo kusini mwa jangwa la Sahara zinazofanya vizuri katika matumizi ya mitandao ya kijamii.

Na hii inachagizwa na ongezeko la watumiaji wa simu janja na huduma ya mtandao (intaneti) nchini.

Taarifa ya Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) inasema watumiaji wa intaneti mpaka kufikia Juni 2021 walikuwa milioni 29 sawa na asilimia 49 ya Watanzania.

Mitandao hii si tu majukwaa ya kimawasiliano, bali ni fursa katika ulimwengu wa leo ya kukuza uchumi wa mtu mmo­ja mmoja na nchi kwa ujumla endapo itatumika vizuri.

Licha ya kuwa na idadi kub­wa ya watumiaji wa huduma za intaneti na simu janja, lakini matumizi ya mitandao ya kijamii yameendelea kuwa kitendawili kwa Watanzania wengi.

Wapo ambao wamekuwa wakiitumia mitandao hiyo kwa namna sahihi ambayo imekuwa ikiwanufaisha kama vile kibiashara, kikazi na kie­limu na wale ambao wameku­wa wakiitumia ndivyo sivyo.

Katika miaka ya hivi karibu­ni, kumeshuhudiwa kukithiri kwa matukio ya upotoshwaji wa taarifa, usambazaji wa maudhui yasiyo na maadili (picha na video za utupu na lugha za matusi) na udhalilish­aji yanayofanywa mitandaoni.

Hii inaashiria kuwa bado kuna kazi kubwa ya kufanya kutokana na kuwepo kwa kundi kubwa la Watanza­nia ambao hawajui kutumia mitandao hiyo kwa malengo ya kunufaika.

Ikumbukwe kuwa matumizi yasiyo sahihi ya mitandao ya kijamii yana athari kubwa kwa ustawi wa jamii ya sasa na hata baadaye kwa kuwa maud­hui yanayopandishwa katika majukwaa hayo zinadumu vizazi kwa vizazi.

Kutokana na kadhia hiyo, TCRA imeamua kuja na kam­peni kabambe iitwayo “Sambaza Mchongo na Sio Uongo” ambayo lengo lake kuu ni kudhibiti ongezeko la matukio haya katika mitandao ya kijamii katika njia ya kubadili­sha mitazamo ya watu juu ya matumizi sahihi ya mitandao hiyo.

Kulingana na Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka hiyo, Dk Jabiri Bakari anasema kuwa kampeni hii inafanyika ikiwa ni sehemu ya jitihada za kuk­abiliana na mwenendo huo ambao umekuwa ukiwaumiza watu wengi.

Kwa upande mwingine, TCRA inajielekeza kuwafun­gulia fursa mbalimbali za kujikwamua kiuchumi watu­miaji wote wa mitandao ya kijamii kupitia kampeni hiyo kama sehemu ya kuhanikiza matumizi sahihi ya mitandao hiyo inayopendwa na maelfu ya watu nchini.

“Kampeni hii ni kubwa na imebeba jumbe kuu nne amba­zo ni; kuzuia usambazaji wa taarifa za uongo na uchoche­zi, uchukuaji wa uhalisia wa mtu mwingine kwa maslahi binafsi, usambazaji wa picha na video za utupu, vurugu au vitisho na Uonevu kwenye mtandao,” Dk Bakari anafa­fanua kuwa ni kosa kuchapi­sha kitu chochote kuhusu mtu mwingine bila ridhaa yake, pia ni muhimu kutoa taarifa kwa jeshi la polisi iwapo utapata shambulio la mtandaoni.

Kulingana na Dk Bakari, katika kipindi hichi cha kam­peni tunaongeza elimu ya matumizi sahihi ya kijitali kwa wananchi na pia tunahama­sisha wananchi wanaonunua bidhaa mitandaoni wanunue bidhaa hizo kwa watu wanaoaminika ili kuepuka kutapeliwa.

“Tutahakikisha kuwa tunatumia watu mashuhuri katika jamii, wahamasishaji, mashuhuda wa matumizi ya mitandao sambamba na vyombo vya habari kupaza sauti kuhusiana na matumizi sahihi ya mitandao ya kijamii,” anaeleza Dk Bakari ambaye anaongeza kuwa hiyo yote ni katika kuhakikisha mitandao ya kijamii inakuwa mahala sal­ama zaidi na fursa kwa wanan­chi.

Imani ya Dk Bakari ni kuwa kampeni hii itafanikiwa kwa ushirikiano mkubwa wa wadau wote wa sekta ya mawasiliano na si mamlaka hiyo pekee, na kupunguza malalamiko ya watumiaji kupitia matu­mizi salama ya mitandao ya kijamii maana ni kosa kisheria kutumia vibaya mitandao ya kijamii.

Shuhuda za wanufaika wa mitandao ya kijamii

Mnufaika wa kwanza

Veronica Kundya ambaye ni mtaalamu wa biashara ya mtandaoni, ni moja kati ya watu wachache walioweza kubadilisha maisha yao kupi­tia biashara ya mtandaoni.

Ni mke na mama wa watoto wawili. Ni mhitimu wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) wa fani ya Sayansi ya Kompyuta.

Bi Veronica anasema safari yake ya biashara mtandaoni ilianzia tangu alipokuwa chu­oni. Baadaye ilichagizwa na msukumo alioupata kutoka katika moja ya mikutano wa biashara ya mtandaoni aliyo­hudhuria kwa kipindi hiko.

“Wakati naanza sikuwa kabisa na mawazo ya kujia­jiri nilikuwa sawa na watu wengine wanaopigiwa kelele wasome hadi chuo kikuu ili waweze kuajiriwa baadaye,” anaeleza Veronica.

Anasema tamanio la kufan­ya lilizaliwa alipokutana na moja ya watu waliomshawishi kufikira biashara hiyo akiwa bado chuoni.

“Wakati naanza biashara, sikuweza kujiamini, niliogopa, na nilichekwa sana, wazazi hawakuelewa na nililia nili­poona hata nilipoanza biasha­ra haikuwa na mwenendo mzuri,” anaeleza.

Bahati nzuri nilikuwa nazungukwa na watu walion­itia moyo, hivyo nilipambana na miezi minne baadaye nilianza kutengeneza kipato cha Sh3 milioni kwa mwezi.

Veronica anadai kuwa hayo yote yamewezekana kutoka­na na kutumia mitandao ya kijamii kwa malengo na si tu kuwasiliana.

“Ili uweze kufanikiwa kutumia mitandao kwa faida ni lazima uwe na malengo na kuzungukwa na watu wana­okusukuma kufikia lengo na si kila mtu,” anaeleza Veron­ica ambaye kwa sasa anapa­ta wafuasi wapya 2000 kwa mwezi mtandaoni.

Veronica kwa sasa ni mjasi­riamali mashuhuri wa bidhaa za kupunguza uzito wa mwili mtandaoni ambaye ameweza kubadilisha pia maisha ya Watanzania wengine wengi kupitia biashara yake hiyo.

Anasema kupitia biashara yake hiyo sasa anaweza kuy­afikia masoko ya dunia nzima bila ya kuwa na duka rasmi.

Mnufaika wa pili

Philip Mbonde ni mjasiria­mali wa utengenezaji keki kwa ajili ya sherehe za harusi, siku za kuzaliwa na matukio mengine.

Baada tu ya kuhitimu masomo yake katika Chuo Kikuu cha Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere (MNMA), Dar es Salaam alifikiria kujia­jiri na kwa kuwa keki ilikuwa ni moja ya vitu anavyovipen­da, ilikuwa rahisi kuanzisha biashara ya keki.

Mwaka 2009, kipindi amba­cho mtandao wa Facebook uli­kuwa gumzo duniani, Mbonde aliutumia kutangaza bidhaa zake za keki.

“Wakati ule, nilikuwa natan­gaza keki zangu katika uku­rasa wangu wa Facebook kwa ajili ya kuwaonyesha watu wangu wa karibu kile amba­cho napenda kufanya lakini haikuwa kibiashara,”anaeleza Mbonde.

Anasema kwa kadri muda ulivyozidi kwenda, kutokana na kuweka keki zake mtanda­oni, watu walianza kuonye­sha uhitaji na hapo akaanza kuutumia mtandao kibiashara rasmi.

“Ujio wa mtandao wa Ins­tagram umesaidia kuongeza wafuasi wangu ambao naami­ni ndiyo wateja pia na mtan­dao huu ni rahisi kufikiwa na watu wengi tofauti na Face­book na mitandao mingine,” anafafanua zaidi.

Mbonde anakiri kuwa matu­mizi sahihi ya mitandao ya kijamii ndiyo yamemuweze­sha kusimama na kufikia hapo ambapo sasa anasambaza keki katika tafrija mbalimbali hapa jijini Dar es Salaam.

“Ukiwa unazungukwa na watu wasio na malengo, watu ambao wanathamini maisha yao tu na si vitu vingine katika mitandao basi hautakuwa na muda kusonga mbele,” ndivyo anavyoamini Mbonde.

Je, una Maswali yoyote juu ya Sekta ya Mawasiliano?
Tuma Mrejesho na Malalamiko!

Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) imejidhatiti kutoa huduma bora kwa wateja na wadau wake wote.

Tuma Mrejesho na Malalamiko!