JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA

MAMLAKA YA MAWASILIANO TANZANIA

TAASISI YENYE VIWANGO VYA ISO 9001: 2015

Mawaziri wa Mawasiliano na Habari Wazindua Mfumo ulioboreshwa wa Leseni TCRA


Mawaziri wa Mawasiliano na Habari Wazindua Mfumo ulioboreshw...

 

Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari Mheshimiwa Dkt. Faustine Ndugulile (Mb) na Waziri wa Habari, Utamaduni Sanaa na Michezo mheshimiwa Innocent Bashungwa (Mb) wamezindua Mfumo ulioboreshwa wa utoaji Leseni wa Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) ambao utawezesha waombaji wa leseni kubwa za mawasiliano kuwasilisha maombi ya leseni kwa njia ya mtandao.

Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari amebainisha kuwa sekta ya Mawasiliano kwa sasa inapitia mabadiliko makubwa na kwamba Serikali imeazimia kufanya mabadiliko makubwa ya uwekezaji katika Teknolojia ya Habari na Mawasiliano TEHAMA na Mawasiliano, na kwamba mfumo huo ulioboreshwa wa uchakataji leseni za Mawasiliano utawezesha upatikanaji wa leseni kwa haraka na kuvutia uwekezaji katika sekta za Mawasiliano,TEHAMA na utangazaji.

“Kwa hiyo na sisi kama Wizara tunaendelea kujipanga kuhakikisha kwamba tunaboresha mifumo yetu ili kuhakikisha kwamba sisi kama wizara hatuwi kikwazo kwao” alisema waziri Ndugulile.

Ndugulile alibainisha kuwa mfumo huo umeboreshwa na kwamba maombi ya leseni ndogo za Mawasiliano kwa akali zitachukua siku tano kuanzia maombi  hadi kukamilika kwa leseni ikiwa mwombaji atakuwa amekamilisha taratibu zote za maombi; kwa upande wa leseni  kubwa zitatumia siku Arobaini na Tano hadi kukamilika hatua ambayo Waziri Ndugulile amesema ni ya kupongezwa kwa kazi kubwa ambayo Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania imefanya hadi kukamilisha kazi ya kuboresha mfumo huo uliobuniwa na kuundwa na wataalamu wa TEHAMA wa TCRA.

“Tunaamini mfumo huu utaongeza uwajibikaji na uwazi kwa sababu kila mmoja atakuwa anaona” alisisitiza Ndugulile na kuongeza.

Waziri Ndugulile alibainisha kuwa Wizara yake kwa pamoja wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo zimeazimia kuhamasisha uwekezaji hasa katika sekta ya Utangazaji hususani katika usikivu wa redio ambapo hivi karibuni wizara ilitoa tangazo la maombi kutoka kwa wananchi wenye nia ya kuwekeza katika utangazaji kwenye wilaya Sitini na Tisa za Tanzania bara.

“Niendelee kutoa rai kwa wawekezaji kwamba sasa hivi tumefungua milango ya uwekezaji katika sekta ya Mawasiliano na TEHAMA ikiwa ni pamoja na mawasiliano ya simu, utangazaji na huduma za posta ambazo tunazisimamia kwa hiyo yeyote anaehitaji kuwekeza tunawakaribisha sana” alisisitiza Ndugulile.

Ndugulile alitumia fursa hiyo kuahidi kwamba Wizara yake inaenda kufanya mabadiliko makubwa katika mfumo wa utoaji leseni sanjari na kufanya mabadiliko ya tozo za leseni zikiwemo leseni za maudhui mtandaoni, huku akibainisha kuwa mabadiliko ya tozo yatakuwa tayari ifikapo mwezi Septemba mwaka huu.

Nae Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Mheshimiwa Innocent Bashungwa alibainisha kuwa wizara anayoisimamia inayo matumaini kuwa mfumo huo wa leseni utaleta mabadiliko makubwa ya kiutendaji hasa katika eneo la uwazi na uwajibikaji.

“mfumo huu unaleta mageuzi makubwa;nimependa ile hali ya uwazi wa mfumo huu wa leseni hii itatusaidia kwenye uwazi ; lengo la wizara hizi mbili ni kuleta ufanisi na kuwa na customer care approach (mrengo wa kuwajali wateja)” alibainisha Waziri wa Habari.

Chini ya mfumo wa utoaji leseni ulioboreshwa; Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) inatoa leseni za aina kuu mbili ambazo ni Leseni kubwa (Individual licence) na Leseni ndogo (Class licence); leseni kubwa zimegawanyika katika makundi yafuatayo Leseni ya vifaa/miundombinu ya mtandao wa Mawasiliano- (Network Facility License - NFL); Leseni ya huduma za mtandao wa Mawasiliano- (Network Services License - NSL); Leseni ya matumizi ya huduma za Mawasiliano- (Application Services License - ASL); Leseni ya maudhui ya Utangazaji (Content Services License  -Televisheni na Redio). Leseni ndogo ni pamoja na Maudhui Mtandaoni (redio na televisheni za mtandaoni, blogu, mitandao ya kijamii na majukwaa mtandaoni); Televisheni za waya (Cable Television); Kuingiza vifaa vya mawasiliano; Kusambaza vifaa vya mawasiliano; Kuuza vifaa vya Mawasiliano; Ufungaji/ujengaji na matengenezo ya vifaa vya mawasiliano; Ungo wa mawasiliano (VSAT); Mawasiliano ya Redio kwenye Ndege; na Mawasiliano ya Redio kwenye Meli. Mwombaji wa leseni anaweza kuwasilisha maombi yake ya leseni kupitia mfumo huo unaopatikana kwenye tovuti ya Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania kupitia kikoa cha www.tcra.go.tz.

Je, una Maswali yoyote juu ya Sekta ya Mawasiliano?
Tuma Mrejesho na Malalamiko!

Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) imejidhatiti kutoa huduma bora kwa wateja na wadau wake wote.

Tuma Mrejesho na Malalamiko!